Advertisement

Responsive Advertisement

DR. HAMIS KIGWANGALLA NA DR. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFURI, KIGWANGALLA AANDIKA UJUMBE MZITO

MAGUFULI NILIYEMJUA, TANZANIA YANGU NA MAPAMBANO! Kigwangalla, huyu X anakusaidia kazi kweli, huyu Y naye anakusaidia? Mbona kuna taarifa zake ziko hivi na hivi na vile?” Ni aina ya simu nilizowahi kupokea mara kadhaa katika maisha yangu ya uwaziri. Simu hizi zilitoka kwa Mhe. Dr. John Pombe Magufuli, Rais wa tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Simu hii ni ya mwisho kunipigia juu ya namna tulivyokuwa tukifanya kazi Wizarani. Alinipigia mwezi wa nne Mwaka 2020, majira ya saa 10 za Alfajir.

Mhe. Dr. Magufuli alipenda akipiga simu moja basi upokee, akirudia ya pili, ukapokea kuwa mnyenyekevu sana na omba msamaha mapema ashushe hasira zake. Akikugundua unanyenyekea basi hujishusha zaidi yako mpaka utaona aibu wewe sasa.

Mbali na Rais Magufuli wanayemzungumzia watu wengi, kuwa alikuwa mkali, havumilii upuuzi na mengine ya namna hiyo, mimi napenda pia kuuelezea upande wake wa upole, huruma na unyenyekevu wa kupitiliza.

Baada ya maswali juu ya mwenendo wa baadhi ya Wasaidizi wangu wa kazi, na mimi kuwakingia kifua, akanimwagia madhambi yao na akanipa maelekezo kadhaa, na mwisho akanionya nisiwaonee huruma, niwaondoe kazini, na kama wako chini ya mamlaka yake, basi nisisite kumpelekea yeye atashughulika nao.

Siku moja niko katika vikao vyangu visivyo rasmi, maeneo ya Southern Sun, hoteli mojawapo kati kati ya jiji la Dar es Salaam, majira ya saa 5 hivi usiku na rafiki zangu akanipigia simu, hii ilikuwa kama wiki mbili toka nimeteuliwa kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, akaniambia hapo ulipo siyo salama. Unatafutwa wewe! Kuna mtu anakuijia hapo sasa hivi, atakupa maelekezo yangu. Umsikilize.

Kweli ghafla nikapigiwa simu nikaambiwa ondoka hapo nenda nyumbani, tunakufuata. Nilishtuka na kuogopa sana. Nikasema nini tena hiki?

Njiani nikasimamishwa, nikapewa ulinzi mpaka nyumbani. Kesho yake nilikuwa nasafiri kwenda nyumbani Nzega. Kufika tu nikakuta mlinzi wangu aliishafika na toka siku hiyo nikawa naye.

Baadaye alikuja kuniita na kuniambia wanaopanga njama dhidi yangu, na akaniambia serikali inawashughulikia. Niondoe shaka.

MAGUFULI NILIYEMJUA...: Na hivyo kila mara, na alinifuatilia kila hatua mpaka baadaye kabisa alipoona tishio dhidi ya maisha yangu limeondoka.

Akasisitiza piga kazi zaidi, wanyooshe. Hii ni nchi yenu nyie vijana, mnapaswa kuipigania. Akasema ‘mimi nimepona majaribio kadhaa ya kuondoa maisha yangu...mpaka nilitaka kuacha kazi ya uwaziri, lakini niliposisitiziwa na Mzee Mkapa kuendelea mbele, na nikakubali, sikuogopa wala kubadili msimamo wangu...wewe songa mbele!’

Alinitia moyo sana kupambana na ujangili, kuimarisha ulinzi wa maeneo yaliyohifadhiwa, kubadili mifumo ya kiutendaji Wizarani, kukuza utalii na mengineyo.

Alipenda sana kuona wewe kama Waziri unafanya kazi yako Kwa weledi na ubunifu wa hali ya juu, alipenda kuona unakimbiza mambo na hausubiri akusaidie ama akufundishe la kufanya. Rais Magufuli alikuwa ni mtu anayetaka kuona matokeo haraka, alipenda kuona Mawaziri wake wanachukua hatua bila kuchelewa. Alipenda kufanya kazi na watu waaminifu na wasio wala rushwa.

Tulipoanzisha mfumo wa kielektroniki wa kukusanya mapato, MNRT Portal, na yeye akajua, alinipigia simu kunipongeza, akasema najua kuna watu wako hapo Wizarani hawataki mfumo huo uanze kutumika kwenye hifadhi zao, waelekeze waanze mara moja, atakayebisha niambie nimtoe.

Rais Magufuli alipenda kuona ukiwa Waziri wake basi unakusanya mapato zaidi kila siku. Aliamini katika kukusanya mapato kwanza, na pili kubana matumizi na kutumia pesa zilizokusanywa kwenye miradi ya kimkakati na kama mmepewa pesa kwa kazi fulani basi mzitumie vizuri.

Alipenda kuziba mianya yote ya matumizi mabaya ya fedha za umma. Alitamani pesa ya serikali ilete thamani halisi kwenye maisha ya watu wake.

Dr. Magufuli alikuwa Mwanafunzi mzuri wa sera na siasa za Mwalimu Julius Nyerere, hususan ile ya Ujamaa na Kujitegemea. Wengine wanajaribu kufananisha.

Rais Magufuli, alitamani kuona nchi inabaki salama, ijitosheleze. Alitamani tujitegemee. Zama za Nyerere ni tofauti na zama za Magufuli. Hivyo mfananisho si rahisi kuuweka, na binafsi sipendi tu, sababu ni ufukunyuku usio na uhalisia wala tija.

MAGUFULI NILIYEMJUA...
Magufuli alikuwa na kipaji cha kuona vipaji na uwezo ndani ya mtu, na akikuamini basi amekuamini. Akikukubali basi amekukubali. Na zaidi urafiki na mapenzi yake kwako ni kama tu ulifanya kazi nzuri Kwa ajili ya Tanzania.

Januari 15, 2020, aliniita ofisini kwake, ilikuwa baada ya kikao. Tukiwa wawili tu aliniambia maneno mengi sana, mpaka machozi yalinitoka. Ipo siku nitayaandika.
Itaendelea...
Dkt. Hamisi Kigwangalla ni Waziri wa Maliasili na Utalii Mstaafu, Mbunge wa Jimbo la Nzega Vijijini. Ni Daktari wa Tiba aliyebobea kwenye Afya ya Jamii.

& Dr. Hamisi Kigwangalla


Post a Comment

0 Comments