LESONI LEO
JUMATATU, AGOSTI 23, 2021
*AMRI YA KUPUMZIKA*
Uumbaji unaweza kuwa ni “mwema sana,” lakini bado haujakamilika. Uumbaji hukoma kwa pumziko la Mungu na baraka za pekee za siku ya saba, Sabato. “Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya” (Mwa. 2: 3),
Sabato ni sehemu muhimu ya uumbaji wa Mungu. Kwa kweli, ndio kilele cha Uumbaji. Mungu anafanya pumziko na kuumba nafasi kwa ajili ya jumuia ambayo wanadamu (katika siku zile familia ya awali ya Adamu na Hawa) wangeacha kazi zao za siku kwa siku na kupumzika wakiwa pamoja na Muumba wao.
Kwa bahati mbaya, dhambi iliingia katika ulimwengu huu na kubadili kila kitu. Hakuna tena ushirika wa moja kwa moja na Mungu. Badala yake, kuzaa kwa uchungu, kazi ngumu, mahusiano yenye kuvunjika upesi na yenye mafarakano, na kuendelea—matatizo yasiyokoma ambayo sote tunayajua vizuri sana kama maisha katika dunia hii iliyoanguka. Na bado, katikati ya yote haya, Sabato ya Mungu inasalia, kuwa alama ya kudumu ya uumbaji wetu na pia tumaini na ahadi ya kuumbwa kwetu upya. Ikiwa walihitaji pumziko la Sabato kabla ya dhambi, kiasi gani zaidi baada ya anguko?
Miaka mingi baadaye, Mungu anapowaweka huru watoto Wake kutoka utumwani Misri, anawakumbusha tena kuhusu siku hii ya pekee.
Soma Kutoka 20:8—11. Hili linatufundisha nini kuhusu umuhimu wa Sabato inavyohusiana na uumbaji?
Kwa amri hii, Mungu anatuita kukumbuka mianzo yetu. Kinyume na kile wengi wanachoamini, sisi sio matokeo ya nasibu ya nguvu zisizothamini na kujali, badala yake, sisi ni viumbe ambao tumeumbwa katika sura ya Mungu. Tumeumbwa ili kuwa na ushirika na Mungu. Haidhuru kwamba Waisraeli walitendewa kama watumwa wenye thamani ndogo. Kwa kila Sabato, kwa njia ya kipekee waliitwa kukumbuka walikuwa nani hasa, viumbe walioumbwa katika sura ya Mungu Mwenyewe.
“Na kwa kuwa Sabato ni ukumbusho wa kazi ya uumbaji, ni ishara ya upendo na uweza wa Kristo.” _—Ellen G. White, The Desire of Ages, uk, 281.`
Fikiria jinsi fundisho la uumbaji wa siku sita lilivyo muhimu. Isitoshe, ni fundisho gani lingine lililo muhimu sana kiasi kwamba Mungu anaamuru kwamba tutenge moja—ya saba ya maisha yetu kila juma, na kwa pamoja, kulikumbuka? Ukweli huu peke yake unapaswa kutufundisha nini kuhusu jinsi ilivyo muhimu kukumbuka mianzo yetu halisi, kama ilivyoelezwa katika kitabu cha Mwanzo?
0 Comments