KESHA LA ASUBUHI
JUMANNE, MEI, 18, 2021
SOMO: UAMINIFU KWA FAMILIA YA BABA
Ili kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe.... Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake.
1 Wakorintho 12:25—27.
Katika Kristo sisi sote ni wanafamilia wa familia moja. Mungu ni Baba yetu, na anatutarajia tuwazingatie wanafamilia wa familia Yake.... Kama matawi ya shina la mzabibu tunapokea virutubisho kutoka katika chanzo kile kile, na kwa utii wa hiari tunakuwa wamoja na Kristo.
Ikiwa mwanafamilia mmoja wa familia ya Kristo anaanguka majaribuni, wanafamilia wengine wanapaswa kumtafuta kwa shauku ya upole, wakitafuta kukamata miguu ambayo inapotea kwenda katika njia mbaya, na kumrejesha katika maisha safi, matakatifu. Huduma hii Mungu anaitaka kutoka kwa kila mshiriki wa Kanisa la Mungu (tazama 1 Wakorintho 12:12—27).
Baadhi kwa sababu hawapokei na kueneza nuru, hawana uzoefu wa kweli wa kiroho. Mara nyingi wanashitukizwa na majaribu yanayokuja katika njia ambayo inavutia sana kiasi kwamba hawayatambui kuwa ni udanganyifu wa adui mwovu. Ni muhimu kiasi gani kwamba wapate uzoefu ambao ni lazima wao wawe nao. Wanafamilia wa familia ya Mungu wanapaswa kuwa na hekima na waangalifu, wakifanya yote kadiri ya uwezo wao ili wawaokoe ndugu zao walio wadhaifu kutoka katika mitego iliyofichika ya Shetani.
Hii ni kazi ya umishenari wa nyumbani, na inawasaidia wale ambao wanaifanya kama inavyowasaidia wale wanaofanyiwa. Shauku ya upole tunayoionyesha nyumbani, maneno ya huruma tunayoyazungumza kwa ndugu na dada zetu, yanatufanya tufae kufanya kazi kwa ajili ya wanafamilia wa familia ya bwana, ambao, ikiwa tutaendelea kuwa waaminifu kwa Kristo, tutaishi nao milele zote.
“Kuwa mwaminifu hata kufa,” Kristo anasema, “nami nitakupa taji la uzima” (Ufunuo 2:10) Basi ni kwa uangalifu kiasi gani wanafamilia wa familia ya Bwana wanapaswa kuwalinda ndugu na dada zao! Kuwa rafiki yao. Ikiwa ni masikini, na wanahitaji chakula na mavazi, wahudumie mahitaji yao ya kimwili vile vile mahitaji yao ya kiroho. Kwa kufanya hivyo utakuwa baraka mara mbili kwao....
Tunapaswa kutenda mambo yetu kwa upole kiasi gani tunapokuwa tunashughulika na wale ambao wanajitahidi kufikia taji ya uzima. Yeye ambaye kwa upendo na upole ameisaidia roho inayohitaji wakati mwingine anaweza kuwa mhitaji wa maneno ya upendo ya kutia matumaini na hamasa.
—Manuscript 63, Mei 18, 1898,, “Kazi ya Umishenari wa Nyumbani.”
0 Comments