Wazazi wapewa onyo kuwalinda Vijana wao Nairobi juu ya Dini ya mashetani iliyoibuka

Polisi wametoa taarifa kuonya kuhusu kundi moja la watu wa kanisa la imani za kishirikina linalowalenga wanafunzi wa Vyuo Vikuu na kuwashauri kuwaua ndugu zao.
Kupitia ujumbe wa Facebook Mkurugenzi wa Idara ya Ujasusi (DCI) Alhamsi, Mei 17, ambao TUKO.co.ke imeusoma, polisi wamewaonya wazazi kuwa waangalifu na watoto wao.
Kuna dini ya imani potofu ambayo imezuka Nairobi inayowalenga wanafunzi wa vyuoni. Ofisi ya DCI inachukua nafasi hii kuonya umma kuhusu dini hii na wazazi kuwa makini sana ili watoto wao wasije wakaingia mtego wa dini hii," sehemu ya ujumbe huo ilisema.
Dini ya mashetani yatua Nairobi, wazazi waonywa
Mkuu wa Polisi Police Joseph Boinett na Mkurugenzi wa kitengo cha Uchunguzi wa Jinai (DCI) George Kinoti. Polisi wametoa tahadhari kuhusu dini potofu Nairobi. Picha: DCI/Facebook.
Kulingana na DCI, dini hiyo kwa jina ‘Young Blud Saints’, inaamini katika miungu watatu.
"Dini hii inaamini kuna miungu watatu wa kweli, mungu asiyekuwa wa kweli na mungu asiye na msimamo. Wanaamini mungu asiyekuwa na msimamo ndiye mungu huwafanya wasifanikiwe kwa kuwa maombi na maamuzi yake sio ya kweli," ujumbe wa DCI uliendelea kusema.
Kulingana na polisi, kundi hilo linatumia changamoto nyingi za vijana kwa mfano kukosa kazi, ndoa zenye misukosuko na umaskini kuwashawishi kujiunga nao kwa madai eti shida hizo zitakwisha.
Dini ya mashetani yatua Nairobi, wazazi waonywa
Mako makuu ya Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Jinai (DCI). Mkurugenzi anawaonya wazazi dhidi ya dini potofu inawashawishi watoto hasa wa vyuoni kujiunga nayo. Picha: DCI/Facebook.
"Wanachama wanaojiunga na dini hii utakiwa kuwaua wanachokipenda zaidi ili kuonyesha uaminifu wao kwa dini hiyo. DCI anafuatilia kwa makini shughuli za dini hii na tunawaomba wazazi na umma kwa ujumla kuwa makini," polisi waliongezea kusema katika ujumbe wao.
Wazazi wametakiwa kuwapeleka watoto wao kwa daktari wa kisaikolojia mara wakitambua tabia isiyokuwa ya kawaida na kuwapa polisi ripoti mara moja ili kusaidia kuimaliza dini hiyo.
Post a Comment